Aondoa zuio la awali la mgao wa mawe
Aelekeza Wachimbaji waruhusiwe na mgawo kuanzia tarehe Machi 26, 2024
Wachimbaji waishukuru Serikali kwa utatuzi wa mgogoro na wenye Leseni za kuchimba dhahabu
Asisitiza wachimbaji wadogo wasiondolewe katika maeneo ya uzalishaji
Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde Machi 25, 2024 alifika katika eneo la Malera Wilaya ya Tarime, Mkoa wa Mara kwa ajili ya utatuzi wa mgogoro baina ya wachimbaji wadogo wamiliki wa leseni na Kampuni ya KIRIBO ambao ulipelekea zuio la mgawo wa mawe mpaka baada ya utatuzi wa mgogoro huo.
Waziri Mavunde alitumia takribani masaa sita kutatua mgogoro husika katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mara kwa kushirikiana na Mkuu wa Mkoa wa Mara, watendaji wa Wizara na viongozi wa wachimbaji wadogo mkoa wa Mara (MAREMA)
“Ni maelekezo ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan juu ya utatuzi wa migogoro mbalimbali katika sekta hii ya madini ambayo inadhoofisha kukua kwa uzalishaji wa madini,” alisema Mavunde
Aidha, alizipongeza pande zote kwa kuridhia makubaliano katika hatua ya awali ya kutatua mgogoro huo.
Aliondoa zuio la mgao wa mawe lililokuwepo hapo awali na kuagiza mgao wa mawe kuanza mapema Machi 26,2024. “Pia, hakikisheni katika utekelezaji wa wa maridhiano haya, wachimbaji wadogo hawaondolewi katika eneo hilo na waachwe waendelee na shughuli zao,” alisema Mavunde.
Akitoa maelezo ya awali, Mkuu wa Mkoa wa Mara Mhe. Said Mtanda alimshukuru Waziri Mavunde kwa kufanikisha utatuzi wa mgogoro husika na kupongeza hatua za kuruhusu mgao wa mawe kwa kuwa hali ya kipato ya wananchi wa eneo hilo ilikwenda chini na mapato ya Serikali kutopatikana kwa wakati.